Home » » MADIWANI BARIADI WANUSA UFISADI KATIKA USHURU.

MADIWANI BARIADI WANUSA UFISADI KATIKA USHURU.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Bariadi, mkoani Simiyu, wametaka kuundwa Tume ya uchunguzi wa mapato yatokanayo na ushuru baada ya kushangazwa na kiasi kidogo cha fedha zilizokusanywa katika minada mikubwa na tegemezi kwa halmashauri hiyo.
Hatua hiyo ni baada ya kupokea na kujadili taarifa ya kamati ya fedha ya kipindi cha robo ya pili ya mwaka wa fedha 2015/2016 ya Oktoba hadi Desemba iliyokuwa ikionesha hali mbaya ya ukusanyaji wa mapato ya ndani.
Taarifa hiyo ilionesha kuwepo kwa baadhi ya minada ambayo ni mikubwa katika halmashauri hiyo na tegemeo yenye zaidi ya watu 7,000, ikikusanya Sh 4,000 hadi 11,000 kama ushuru wa matandiko, ng’ombe na mazao mchanganyiko kwa muda wa mwezi mmoja.
Madiwani hao walionekana kushangazwa na hali hiyo wakati wa kikao cha baraza la halmashauri kilichofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita, na walidai kwa nyakati tofauti kuwepo kwa vitendo vya rushwa katika ukusanyaji huo.
Kwa mujibu wa madiwani hao, minada mikubwa ya Dutwa, Nkololo, Masewa na Ngulyati ambayo ni tegemeo kubwa kwa halmashauri hiyo, inaonesha imekuwa ikikusanywa Sh 4,000 hadi 11,000 mara nne katika kipindi cha mwezi mmoja huku mingine ikiwa haina kiasi chochote cha fedha kilichokusanywa.
Walisema haiwezekani minada hiyo na mingine, pamoja na magulio zaidi ya 20, ikusanye kiasi kidogo kama hicho, huku wakieleza kuwa wamekuwa wakishuhudia zaidi ya tani 300 za mazao mchanganyiko zikibebwa katika magari.
“Hapa kuna baadhi ya watumishi ambao ni wahusika katika ukusanyaji wa ushuru, kodi hizi zinaishia katika mifuko yao lazima uchunguzi ufanyike haiwezekani katika mnada au gulio yakusanywe matandiko ya watu wawili, magunia yatozwe mawili pekee,” alisema Benjamin Holela.
Diwani wa Girya, Lewa Safari alisema amekuwa akishuhudia katika minada ya Dutwa na mingine zaidi ya tani 300 za mazao na ng’ombe 600 vikitolewa ndani ya mnada huo lakini anashangazwa kuona kiasi kidogo kilichokusanywa.
Alisema kuwa baadhi ya minada na magulio imekuwa haina mawakala na hivyo halmashauri kupitia idara ya fedha hulazimika kukusanya yenyewe, ambapo alisema inashangaza gari kuwekwa mafuta na watu kulipwa posho kufuata ushuru, lakini wanarejea na kati ya Sh 4,000 na 11,000.
Akizungumzia hali hiyo Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Abdallah Malela, alisema baadhi ya minada na magulio imekuwa na migogoro mikubwa, hali inayoisababishia halmashauri kutokukusanya ushuru kabisa na wakati mwingine kukusanya kiasi kidogo.
Aidha alisema minada mingi na magulio vipo chini ya halmashauri lakini havina mawakala kutokana na baadhi yao kuvunja mikataba kwa kushindwa kufikia kiwango cha makubaliano ya ukusanyaji wa ushuru katika mikataba yao.
CHANZO ; HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa