Home » » WAIGIZAJI VAENI UHALISIA

WAIGIZAJI VAENI UHALISIA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Ni wazi kuwa kila moja wetu anatamani kuburudika bila kujali ni aina gani ya burudani anayotaka.
Kuna aina nyingi na tofauti za burudani. Kuna muziki wa taarabu, Injili, dansi, wa kizazi kipya hata muziki wa kiasili.
Katika kundi la burudani pia kuna sanaa za maonyesho, ngoma, vichekesho hata filamu. Hizo ni baadhi ya burudani na kila mmoja ana uchaguzi au mapenzi yake kwa aina moja au zaidi.
Lengo langu leo ni kuzungumzia burudani lakini nikilenga zaidi upande wa filamu. Hapa nawapongeza waigizaji kwa kazi nzuri. Tasnia inakuwa kila kukicha na mabadiliko yanaonekana ingawa siyo kwa asilimia kubwa.
Mabadiliko kwa nchi inayoendelea kukua kama Tanzania yanakuja taratibu, hivyo hata katika nyanja hiyo kasi ya ukuaji wake ni hiyo hiyo.
Hata hivyo, naweza kusema kuwa mabadiliko yapo na kwa anayefuatilia anaweza kuona baadhi ya waigizaji walivyobadilika.
Ingawa tunajivunia kukua kwa filamu, lakini katika kazi hiyo sasa, badala ya kulipeleka mbele gurudumu hilo, tunafikiria kulirudisha nyuma. Sababu kubwa ya kulirudisha nyuma gurudumu la filamu ni aina ya uigizaji na jinsi tunavyojichanganya katika uhalisia. Filamu nyingi zinaigizwa bila kuonyesha uhalisia wa kilichokusudiwa.
Haiwezekani mwanzo hadi mwisho wa filamu azungumziwe mtoto bila kuonekana hata katika kipengele kimoja. Hilo linatokea kwenye filamu, huku wazazi wakilitumia jina lake katika mazungumzo yao, wala hawasemi kama amesafiri au la.
Filamu bora ni ile yenye uhalisia, mtu anaposema yupo kijijini, aonekane kweli yupo huko. Ni ngumu kuamini unapomwona mhusika amekuja kutafuta kazi kwa mara ya kwanza mjini, lakini ametinda nyusi na kubandika kucha. Akili yangu inanituma kuwa, filamu haiigizwi usiku mmoja. Ni kitu kinachoandaliwa kwa muda mrefu, hivyo kuna haja ya kuwa na maandalizi ya uhalisia hata ikibidi kufuga ndevu ikiwa zitahitajika.
Msichana anapoigiza kuwa ametoka kijijini, asitinde nyusi au kuvaa wigi. Ajiandae na kuonyesha uhalisia wa maisha ya kijijini. Ni muhimu kufanya maandalizi ya kitu kilichopo mbele yake ili kuvaa uhalisia akiaminisha mashabiki .
Kuna wakati moja ya filamu za bongo ilizua gumzo kwenye mitandao ya kijamii. Ilionyesha mtu aliyeigiza ujambazi, eti anavua viatu ili aingie ndani ya nyumba kufanya ujambazi. Jambo hilo ni ajabu kuruhusiwa na watayarishaji wa filamu ikizingatiwa mazingira halisi pale unapofanyika ujambazi.
Kuruhusu hali hiyo iende na kuonekana kwa mashabiki au wateja wa filamu ni kuwaibia. Hiyo yote inaonyesha wengi wa wasanii wanavyoshindwa kuuvaa uhusika. Kwa bahati mbaya filamu hiyo ilihaririwa na kuwa tayari kwa ajili ya kuwafikia watazamaji na wadau wa kazi hizo. Lakini jambo la kujiuliza; je, kazi ya wahariri wa filamu ni ipi kama wanapitisha vitu kama hivi?
Nawahurumia kwa kuwa mwisho mnaubeba udhaifu wenu wazi mbele ya jamii mnayotaka kuifunza, kuiburudisha lakini pia ninyi kupata kipato kwa mauzo ya kazi zenu. Kataeni aibu hii kwa pamoja kwa kuwa ili malengo yenu yatimie ni lazima tasnia hii iwepo na iwe na heshima. Lakini kama mtashindwa kuilinda, mjiandae kutafuta kazi nyingine kwani hii itakuwa imekwisha.
Hakuna atakayekubali kutupa fedha kila siku kuangalia filamu zisizo na uhalisia. Haina ubishi kuwa, kinachoonekana kwa wakati huo ni filamu iliyoigizwa sawa, lakini kutokana na mabadiliko yaliyopo kwenye nyanja hiyo ni lazima kuwapo na uhalisia. Kuigiza filamu bila kuwa na uhalisia ni kujiweka nyuma kwani upinzani uliopo sasa katika nyanja hiyo ni mkubwa kutokana na dunia kuwa kijiji.
Tunakokwenda katika tasnia ya filamu, mwanga wa mafanikio upo. Ni wakati wenu kuwa makini kabla hamjaleta aibu sebuleni kwa wadau wenu.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa