Home » » UNACHOTAKIWA KUFANYA ILI UWE NA NDOA YENYE AMANI-2

UNACHOTAKIWA KUFANYA ILI UWE NA NDOA YENYE AMANI-2

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Kama unaingia kwenye ndoa kwa sababu ya kumkera fulani, fahamu kwamba hilo ni kosa na linasababisha wakati fulani watu kujuta kwanini amekutana na fulani.
Ingawa watu wanaweza kusema kwa kadri wanavyoweza, ukweli ni kwamba utulivu kwenye ndoa kwa asilimia kubwa huletwa na mwanamke. Utulivu huzaa mapenzi na huruma baina ya wanandoa, kwa maana nyingine, mwanamke ana nafasi kubwa ya kujenga au kubomoa ndoa, hii haina maana yake ni kwamba mwanamume hana nafasi ya uharibifu, bali nafasi ya mwanzo inachukuliwa na mwanamke bila ya upinzani.
Sababu kubwa ya wanandoa kuchokana, au kuzeeka kwa ndoa kunasababishwa na mwanamke, pale ambapo atashindwa kutumia nafasi yake na vipawa alivyopewa kuleta utulivu katika ndoa yao, na hapa nitajaribu kujadili baadhi ya visababishi vinavyopelekea kuzeeka kwa ndoa au kuchokana. Visababishi ambavyo huwa vinadharaulika na kuonekana vitu vidogo vidogo hususan kwa wanawake wengi.
Wapo ambao wanaweza kukanusha hili, lakini unapaswa kujiuliza inakuwaje kama kweli mwanaume anashiba, kwanini aende kusaka wanawake wengine kwa ajili ya kufanya nao ngono. Huenda akawa na sababu nyingine, hata hivyo kwa asilimia kubwa hiyo humaanisha kwamba huenda ndani ya ndoa yake kuna shida, hasa ya kupata kile ambacho anakwenda kukitafuta nje.
Kuna wanawake wengi wamekuwa wakiwanyanyasa wanaume kwa kauli zisizo nzuri…kama jana nilikupa na leo unataka kwani mimi sichoki…nk. Ingawa inaonekana kama ni suala lisilo na maana, lakini zungumza na wanaume wengi ambao wametoka tayari nje ya ndoa, mojawapo ya sababu ni kutokuwa na uhakika wa kushiba katika ndoa zao. Hawapati raha ile ambayo wanandoa wanastahili kupewa.
Kuna wanandoa wamekuwa wanaishi isivyo sawa, kwamba wanaishi bila kuelewana vizuri. Kuelewana baina ya wanandoa ni suala la msingi sana. Matatizo mengi ndani ya nyumba yanaweza kusababishwa na moja au baadhi ya tabia za baadhi ya wanandoa, kwamba mwingine anakuwa hana ukaribu au anafanya mambo ambayo hayamfanyi mmoja kati yao kutokuwa na amani moyoni.
Wanapoanza uhusiano mwanamke kwa mwanaume, hujali sana kuvaa vizuri, usafi wa mwili wake, usafi wa nyumba na nidhamu ya hali ya juu. Aidha huwa ni kawaida kwa mwanamke kumuuliza mwenzi wake anapenda kipikwe chakula gani na kadhalika. Hata hivyo kadri siku zinavyokwenda mbele, si wanawake wengi huona umuhimu wa kuwauliza wenza wao chakula cha kupika.
Wengi hupika chakula bila kuzingatia vionjo vizuri wala kuwa na ubunifu. Wengine wamekuwa hawana mapokezi mazuri kwa wenza wao. Lini uliwahi kumpokea mwenzi wako kwa kumpokea kwa kumkumbatia? Kila aliyeko kwenye ndoa anapaswa kujiuliza hili.
Kuweni na mazungumzo
Mazungumzo ni njia muhimu ya kujenga ndoa na kuiimarisha , aidha ni njia ya mkato ya kuchokana na kuchukiana. Mwanamke ambaye hajui wakati gani aseme nini na wakati gani asiseme, hujikuta katika wakati mgumu ndani ya ndoa yake.
Kama una mwanamke wa namna hii ambaye kila anapoongea na mume wake huanza mazungumzo yake na matatizo na lawama humfanya mumewe awe na woga kila anaposikia sauti yake, na kuiona nyumba chungu, kwa sababu hakuna binadamu anayependa kusikia matatizo tu wakati wote.
Ukweli mwanamke wa aina hii huwa anamsubiri mumewe kwa hamu kubwa, na anapofika tu na kabla hata ya kupata rizki, anaanza kumsomea orodha ya matatizo; watoto wamerudishwa shule, karo haijalipwa, shangazi yako amepiga simu mjomba kalazwa Hospitali na kadhalika na kadhalika. Nyumba ya aina hii huzeeka haraka na wanandoa kuchokana

Udhaifu mkubwa
Ni udhaifu mkubwa kwa wanandoa, kwamba baadhi yao wamekuwa hawasomani na kujuana tabia. Bahati mbaya zaidi kuna wanandoa ambao wamekuwa wakitaka tabia zao ndizo ziwe za kufuatwa katika ndoa hata kama siyo nzuri. Kama unataka maisha mazuri ya ndoa, hakikisha unaisoma tabia ya mwenzi wako na kujua na kwenda naye. Msingi wa kuwa na maisha bora ya ndoa ni pamoja na kuifahamu kwa kina tabia ya mwenzi wako na kuchukua hatua muafaka zenye lengo la kuimarisha uhusiano wenu.
Kwa mwanamke mwenye busara na mwenye kuithamini ndoa yake, husoma tabia za mumewe na kuangalia jinsi gani anavyoweza kuzioanisha na zile zake ili kuepusha migongano, aidha hutafuta fursa muafaka ya kumkinaisha mumewe juu ya fikra fulani au tabia fulani ambayo yeye haridhiki nayo. Ni muhimu kwa mwanaume vilevile kuzisoma tabia za mke wake, vitu gani vinamuudhi, na vitu gani vinamfurahisha.
Katika ujenzi wa ndoa imara, kuna vigezo vingine ambavyo si muhimu lakini havipaswi kupuuzwa, miongoni mwa vigezo hivyo ni kiwango cha wanandoa kijamii na kiuchumi, hiki ni kigezo ambacho kinaweza kuonekana ni cha kidunia zaidi, lakini uzoefu unaonyesha kuwa kimekuwa ni miongoni mwa sababu zinazopelekea chokochoko katika familia na hatimae kuikwaza ndoa yenyewe.
Inapotokea kwa mmoja miongoni mwa wanandoa hususan mwanamume akawa na hali duni kiuchumi kuliko ile ya mkewe (familia ya mkewe) basi pamoja na mapenzi yanayowaunganisha, maisha yao yatakuwa na tahadhari kubwa sana, na wakati wowote kinaweza kutokea kitu ambacho hakikutarajiwa na kikazua mtafuruku.Ni vema wanandoa wakaanza kujenga misingi imara ya ndoa yao kwa kujitahidi kuzingatia kigezo hiki cha Kiuchumi na Kijamii
Wapo watu wanaosema kwamba elimu siyo jambo la msingi. Hata hivyo hilo siyo sahihi. Inapokuwa elimu ya mwanamke ni kubwa kuliko ya mwanamume, kwa mfano, mwanamke anapokuwa na shahada ya Chuo Kikuu, na mwanaume ya Darasa la Saba, hapa panahitaji hekima na juhudi kubwa kwa mwanamke kuweza kumuelimisha mumewe bila ya kumfanya ajihisi mjinga, zoezi ambalo ni gumu, na uwezekano wa kushindwa ni mkubwa.
Aidha kuna suala la wanandoa kuishi karibu na ndugu. Ndoa za ndugu wa karibu, zinaweza zikawa ni sababu ya kuimarika kwa ndoa au sababu ya kudhoofika, lakini kwa uzoefu wetu imeonekana kuwa ndoa za aina hii mara nyingi zinafikia katika hatua ya uzee mapema zaidi, hii ni kutokana na kufahamiana kwa ndugu hawa tangu utotoni, na kila mwanandoa kutotarajia jipya kutoka kwa mwenzake
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa