Home » » DC MASWA AZINDUA WIKI YA CHANJO

DC MASWA AZINDUA WIKI YA CHANJO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Na Samwel Mwanga-Maswa
 
MKUU wa wilaya ya Maswa mkoani Simiyu,Luteni Mstaafu Abdalah Kihato
amezindua wiki ya chanjo jana katika halmashauri ya wilaya hiyo na
kuwahimiza wananchi kuona umuhimu wa kuwapeleka watoto wote kupata
chanjo wanazostahili.
 
Uzinduzi huo ambao ulihudhuriwa na wananchi wachache umefanyika katika
zahanati ya Malita kata ya Zanzui kwa kuzindua chanjo za
kuhara(Rotavirus)na Nimonia(PCV 13) kwa watoto wa chini ya mwaka
mmoja.
 
Alisema kuwa chanjo iliyokamilika ndiyo msingi wa kuwa na afya njema
kwa sababu mwili utakuwa na kinga ya maradhi kwa miaka mingi.
 
“Watoto ni binadamu dhaifu sana wanahitaji uangalizi wa karibu na wa
hali ya juu sana maana katika maisha yao hawana wanachokijua isipokuwa
titi la mama kwa hiyo wanahitaji sana huduma ya chanjo iliyokamilika
ili waishi na kuimarika kwa afya zao”alisema.
 
Pia  amewataka wazazi kuwapeleka watoto wao kwenye vituo husika ili
kupatiwa chanjo hizo huku akiwataka kutoa taarifa endapo muuguzi
yeyote atawatoza fedha wakati wa chanjo hizo kwani  zinatolewa bila
malipo yoyote.
 
Awali mganga Mkuu wa wilaya ya Maswa,Dr Jonathan Budenu alisema kuwa
kiwango cha ufanisi kwa chanjo ya Pentavalent 3 inayozuia magonjwa
matano ambayo ni Kifaduro,Dondakoo,Pepopunda,Homa ya Ini na Homa ya
Uti wa mgongo kimeongezeka kutoka asilimia 82 mwaka 2012 hadi asilimia
93 mwaka 2013.
 
“Katika wilaya yetu ya Maswa kiwango cha ufanisi kwa chanjo ya
Pentavalent 3 kimeongezeka kwani mwaka 2012  hadi 2013 watoto 18,481
walichanjwa kati ya watoto 19,807 na hawa chini ya umri wa miaka
mitano”alisema.
 
Dr Budenu pia alieleza kuwa wamekuwa wakipambana na changamoto
mbalimbali katika utekelezaji wa zoezi hilo ambazo ni pamoja na uelewa
mdogo wa jamii kuhusu umuhimu na ukamilishaji wa chanjo zote,watoto
wapatao 1326 hawakupata au kukamilisha chanjo na ukosefu wa usafiri
kwa ajili za kliniki za mkoba za chanjo kwa baadhi ya vituo vya
kutolea huduma za afya.
 
Ujumbe wa Wiki ya Chanjo wa mwaka huu ni Jamii iliyokamilisha chanjo
ni jamii yenye afya wenye kauli mbiu isemayo”Chanjo ni jukumu letu
sote”.
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa