Home » » Walimu Maswa wamkataa Ofisa Elimu

Walimu Maswa wamkataa Ofisa Elimu

WALIMU wa shule za msingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, mkoani Simiyu, wamemtaka mkurugenzi na mwenyekiti wa halmashauri hiyo kumwondoa Ofisa Elimu wa Shule za Msingi wilayani humo, Mabeyo Bujimu kwa madai ya kuwa kikwazo katika utendaji kazi wa idara hiyo.
Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Maswa jana, walimu hao walisema wameamua kuchukua uamuzi huo kutokana na tuhuma mbalimbali zinazomkabili ofisa huyo, kwani wamebaini vitendo anavyofanya vinaweza kukwamisha mikakati iliyowekwa na wilaya hiyo kuinua taaluma.
Walisema amekuwa akitumia lugha chafu kwa walimu huku akiwatishia, hasa walimu wanaofundisha maeneo ya mjini kuwa atawahamishia shule za vijijini, hali inayotoa tafsiri kuwa wanaofundisha vijijini ni kama wamepewa adhabu.
“Huyu Ofisa Elimu amekuwa akitembelea katika shule na kututisha sisi walimu kuwa atatuhamishia shule za vijijini, na hivi karibuni alifuta kwa mdomo uhamisho wa mwalimu Hadija Shwaibu aliyekuwa amehamishiwa Shule ya Msingi Nghami na kumrejesha Shule ya Msingi Hinduki huku akimtuhumu Ofisa Elimu Taaluma, Patrick Musira alipokea rushwa na kutoa uhamisho huo jambo ambalo si kweli,” alisema Said Juma.
Pia walimtupia lawama kwa kutumia nafasi yake kuwataka kimapenzi walimu wa kike sambamba na kuwateua  kwa upendeleo.
Walisema mbali na tuhuma hizo amekuwa akitumia vibaya gari la idara lenye namba za usajili SM 4708.
Mbali na hayo walilalamikia kitendo cha kutoa amri kwa walimu wa Shule ya Msingi Binza kuwazomea walimu wa Shule ya Msingi Shanwa kwa madai kuwa hawakufanya vizuri katika matokeo ya mtihani wa darasa la saba mwaka jana, hali ambayo imewavunja moyo walimu waliozomewa.
Akizungumzia tuhuma hizo, Ofisa Elimu huyo, Mabeyo alisema anafahamu chanzo cha malalamiko hayo kinatokana na kusitisha uhamisho wa baadhi ya walimu bila barua, ambao anadai ulitolewa kinyemela na maofisa wenzake.
Hata hivyo, alipotakiwa kuyatolea ufafanuzi malalamiko mengine, alikataa hadi atakapowasiliana na  Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Hilda Lauwo.
“Haya malalamiko yote na hata kuitwa kwa waandishi wa habari kunihoji hapa kunatokana na mimi kusitisha uhamisho kwa baadhi ya walimu waliopewa uhamisho kinyemela kutoka ofisini kwangu, haya mengine labda niwasiliane na mkurugenzi, akikubali basi nitayajibu na kuyatolea ufafanuzi mbele ya wenzangu,” alisema.
Hata hivyo, alipotakiwa na waandishi wa habari kujibu tuhuma zinazomhusu yeye mwenyewe kama vile kuwa na mahusiano ya kimapenzi na walimu wa kike kwa kutumia madaraka yake, alipata kigugumizi na kusisitiza kuwa hadi aonane na mkurugenzi.
Chanzo; Tanzania Daima

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa