Home » » Meatu waanzisha miradi ya umwagiliaji

Meatu waanzisha miradi ya umwagiliaji

Katika kukabiliana na tatizo la ukame wa mara kwa mara,Halmashauri ya Wilaya ya Meatu mkoani Simiyu inakusudia kuanzisha miradi ya kilimo cha umwagiliaji katika maeneo mbalimbali wilayani humo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa hivi karibuni na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo ya wilaya,John Wanga katika kikao cha Baraza la madiwani lengo la kuanzishwa kwa miradi hiyo ni kuwawezesha wakazi wa wilaya hiyo kukabiliana na tatizo la uhaba wa chakula kila mwaka.
"Kutokana na hali ya ukame wilaya imetambua njia pekee ya kuwa na uzalishaji wa uhakika ni kuimarisha kilimo cha umwagiliaji. Mkazo umewekwa zaidi katika maeneo yanayofaa kwa kilimo hiki, maeneo yote yana jumla ya hekta 2,145 yaliyopo katika vijiji vya Mwagwila, Usiulize, Mwakasumbi na Tindabuligi," alieleza Wanga.
Wanga alisema hivi sasa halmashauri yake tayari imeanza mchakato wa utekelezaji waskimu ya umwagiliaji katika Kijiji cha Usiulize itakayokuwa na ukubwa wa hekta 245 ambapo
tayari andiko na michoro ya mradi huo vimeishakamilika na kinachosubiriwa ni fedha kiasi cha shilingi bilioni nne.
Akifafanua Wanga alisema skimu ya umwagiliaji katika Kijiji cha Mwagwila uliopo katika Bonde la Mto Semu ina ukubwa wa hekta 150 ambapo
itakapokamilika ujenzi wake inatarajiwa wakulima wapatao 350 watanufaika na mradi huo.
Hata hivyo, alisema katika maeneo yote hayo kilimo hicho cha umwagiliaji kitatekelezwa na
wakulima wadogo kwa kutumia pampu za kusukuma maji pamoja na ndoo na hivyo kuwawezesha kulima kwa wingi mazao ya chakula, mbogamboga na matunda ambayo yatawaongezea vipato vyao baada ya kuuza.
Ofisi yangu kwa ushirikiano wa ofisi ya mkuu wa wilaya tutahakikisha wakulima wote katika maeneo yenye skimu hizi wanazingatia masharti ya kilimo bora na ili kuhakikisha panakuwepo mafanikio tumeunda timu za viongozi na wataalamu wa kilimo zitakazosimamia utekelezaji kuanzia ngazi ya kata hadi wilaya, alisema Wanga.
Katika hatua nyingine Wanga aliwaomba madiwani wa halmashauri hiyo ya wilaya kuwahimiza wakulima katika kata zao kuhakikisha wanapanda mazao yanayostahimili ukame kama vile uwele na mtama ili kukabiliana na tatizo la ukosefu wa chakula mwakani kutokana na hali ya hewa kuonesha huenda mvua za masika zisinyeshe kwa kipindi kirefu.

Chanzo;Majara

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa