Home » » Maswa wataka Pinda amtimue mkurugenzi

Maswa wataka Pinda amtimue mkurugenzi

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Hilda LauwoWANANCHI wilayani Maswa, Simiyu, wamemtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kumwondoa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Hilda Lauwo, kwa madai hana uwezo wa kuongoza halmashauri hiyo.
Wananchi wamefikia hatua hiyo kutokana na tuhuma mbalimbali zinazomkabili zikiwemo za matumizi mabaya ya fedha za halmashauri, matumizi mabaya ya madaraka na kauli chafu kwa wananchi na watumishi walioko chini yake.
Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Maswa baadhi ya wananchi walisema tangu ahamishiwe katika wilaya hiyo akitokea wilaya ya Ludewa alikokataliwa na madiwani amekuwa ni mzigo.
Walieleza amekuwa akitumia vibaya madaraka yake kwa kuchota mamilioni ya fedha za safari zikiwemo fedha za mafuta ya gari sambamba na posho ya dereva, lakini haendi safari.
“Kwa kuonyesha alivyo mbadhirifu wa fedha za halmashauri Mei 27 mwaka huu alichukua sh milioni 3 kwa ajili ya kuhudhuria kikao cha Lake Victoria Region Local Authorities Cooperation(LVRLAC) kilichofanyika jijini Kigali, Rwanda Mei 29, lakini hakuhudhuria kikao hicho baada ya kuzuiwa na Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu na hivi karibuni amechukua sh milioni 2 kwa ajili ya kuhudhuria mafunzo ya wiki mbili ya kompyuta kwa wakuu wa idara jijini Mwanza lakini akaenda mjini Entebe, Uganda, kuhudhuria kikao cha LVRLAC,” alisema mmoja wa watumishi wa halmashauri hiyo.
Walieleza kuwa mkurugenzi huyo amekuwa na safari za mara kwa mara huku ofisi yake akiacha kaimu ambaye hawezi kutekeleza majukumu kutokana na kutokuwa na maamuzi ya kutosha huku akitumia gari la halmashauri SM 4135 Landcluser VX  kubebea pumba za nguruwe kutoka Maswa hadi nyumbani kwake wilayani Korogwe, Tanga.
Hata hivyo, walitoa lawama kwa mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Stephen Dwese, kuwa amekuwa akimkumbatia licha ya malalamiko dhidi yake.
Akizungumzia malalamiko hayo kwa njia ya simu, mkurugenzi huyo alisema safari anazozifanya mara kwa mara huwa zina baraka kutoka kwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na wanaolalamika wana chuki binafsi naye.
Hata hivyo alipotakiwa kutolea ufafanuzi wa tuhuma zingine zinazomkabili alikata simu na alipotafutwa simu yake haikupatikana tena.
Chanzo;Tanzania Daima

1 comments:

Unknown said...

kiukweli anatakiwa afukuzwe ili liwe onyo na fundisho kwa watu wengie wenye tabia na mwenendo kama wake

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa