Home » » Mashindano ya Serengeti Marathon mwaka 2013 yamalizika, Wakenya watwaa zawadi za juu

Mashindano ya Serengeti Marathon mwaka 2013 yamalizika, Wakenya watwaa zawadi za juu

MASHINDANO ya Serengeti Marathon mwaka 2013, yamemalizika katika wilaya ya Busega, mkoani Simiyu, na washindi kukabidhiwa zawadi zao, ikiwemo zawadi ya juu ya shilingi milioni 2.5. Mashindano hayo yaliyoandaliwa na mkurugenzi wa Serengeti Marathon, ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Busega, na mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM), mkoani Simiyu, Dk. Titus Kamani, yameshirikisha wakimbiaji kutoka ndani na nje ya nchi. Akimkaribisha mkuu wa mkoa wa Simiyu, Paschal Mabiti kwa ajili ya kutoa zawadi na kufunga mashindano hayo, Dk. Kamani amesema kuwa yalikuwa ya mbio za kilomita 42, 21 na tano kwa wazee na kwamba yalianzia katika hifadhi ya taifa ya Serengeti na kumalizikia katika eneo la Stop Over, lililoko jirani na hifadhi hiyo katika kijiji cha Lukungu wilayani Busega. Amesema kuwa washiriki wa mashindano hayo walikuwa wametoka katika mikoa ya Singida, Mwanza, Mara, Arusha, Kilimanjaro, Dar es salaam, Tabora na wenyeji Simiyu, pamoja na wengine kutoka nchi za nje za Kenya, England na Sweden na kwamba yalishirikisha wanaume kwa wanawake. Amesema kuwa lengo la mashindano hayo ni kuhamasisha uhifadhi, kupiga vita ujangili na kutangaza utalii, ambapo kauli mbiu ya mwaka huu ni kupig vita ujangili wa wanyama pori katika hifadhi zetu. Akitoa zawadi kwa washindi mkuu wa mkoa wa Simiyu Mabiti, kwa niaba ya waziri mkuu Mizengo Pinda, alimpongeza Dk. Kamani kwa kuanzisha mashindsano hayo kwani yana lengo zuri la kulinda hifadhi na kutangaza utalii. Aidha, ameongeza kuwa pia mashindano hayo kwa namna moja pamoja na kuwa ajira kwa washiriki, lakini pia yanadumisha ushirikiano, umoja na upendo kwa washiriki ambao wanatoka maeneo mbalimbali wakiweo wageni kutoka nje ya nchi na kwamba pia yanadumisha ushirikiano wa Afrika mashariki. Mabiti amewataka washiriki wa mashindano hayo hasa waliotoka nje ya nchi kuwa mabalozi katika nchi zao kwa kutangaza nchi yetu katika suala zima la utalii na vivutio vilivyopo ambavyo ni vingi sana. Aidha, amewataka wananchi wa wilaya ya Busega na mkoa wa Simiyu kwa ujumla, mwakani kujitokeza kwa wingi kwenye mashindano hayo, ili waweze kujinyakula zawadi. Washindi katika mashindano hayo walikabidhiwa zawadi ya fedha tasilimu kuanzia sh. 20,000 hadi shilingi milioni mbili na nusu, na medali za fedha, ambapo wakimbiaji kutoka nchini ya Kenya walionekana kung’ara na kukamata nafasi za juu, wakifuatiwa na wa mikoa ya Arusha na Manyara, na pia wenyeji wa wilaya ya Busega waliibuka washindi na kukabidhiwa zawadi. Mashindano ya Serengeti Marathon yalianza rasmi mwaka jana na yamekuwa yakifanyika kila mwanzoni mwa mwezi wa desemba katika wiki ya kwanza. Wadhamini wa mashindano hayo mwaka huu walikuwa ni pamoja na Grumet Fund Tanzania, Coca cola, WWF, Hifadhi za taifa (Tanapa), Serengeti Breweries, NSSF, Hifadhi ya Serengeti na Board Of Trusrees.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa