Home » » Watumishi waliofukuzwa kazi kwa wizi, rushwa warejeshwa kazini

Watumishi waliofukuzwa kazi kwa wizi, rushwa warejeshwa kazini

WATUMISHI wanne wa halmashauri ya wilaya ya Busega, mkoani Simiyu, waliokuwa wamefukuzwa kazi na madiwani mwaka jana kutokana na tuhuma mbalimbali, ikiwemo ya ubadilifu wa fedha za mahindi ya msaada, pamoja na kukamatwa na rushwa na Takukuru, wamerudishwa kazini baada ya kukata rufaa.

Watumishi hao ambao watatu ni maafisa watendaji wa vijiji na mmoja afisa mtendaji wa kata, jana wamethibitishwa  kurudishwa kazini kwenye kikao cha kwanza cha baraza la madiwani wa halmashauri ya wilayaya Busega, kilichofanyika katika mji mdogo wa Lamadi wilayani humo.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya mpya ya Busega, Bw. John Lukale, amesema kuwa watendaji wawili walikamatwa na takukuru kwa tuhuma ya kuomba rushwa na wengine walikamatwa wakiwa wamefuja fedha za mahindi ya msaada yaliyotolewa serikali kwa ajili ya kuuzia wananchi kwa bei nafuu.

Bw. Lukale amesema kuwa kufuatia hali hiyo watumishi hao walifukuzwa kazi baada ya kubainika kwamba wanayo makosa.

Amesema kuwa baadaye watumishi hao walikata rufaa katika utumishi wa umma, na ikaamriwa warejeshwe kazini na kwamba kwa jinsi hiyo, baraza la madiwani sasa limethibitishwa kurejeshwa kazini.

Wakichangia hoja hiyo madiwani hao wamesema kuwa pamoja na watendaji hao kurejeshwa kazini, ni vema sasa wabadilishiwe vituo vya kazi kwa sababu wananchi wa maeneo husika hawana imani nao tena, lakini pia hali hiyo ni kwa ajili ya usalama wao.

Kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Busega, Bw. Pamphil Masashua, amewataka watendaji wote kufuata miiko na maadili ya kazi yao, vinginevyo hatua za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Katika kikao hicho mkuu wa wilaya ya Busega, Bw. Paul Mzindakaya, amewataka  madiwani na watendaji wote wa serikali wilayani humo kushirikiana na kuwa kitu kimoja, ili kuharakisha maendeleo katika wilaya hiyo mpya.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa