Home » » DC Kihato ahimiza usafi Wilayani Maswa

DC Kihato ahimiza usafi Wilayani Maswa

Mkuu wa wilaya ya Maswa, mkoa wa Simiyu, Luteni mstaafu, Abdalah Kihato, amewaagiza viongozi wote wilayani humo kuhakikisha kuwa wananchi wanafuata kanuni za usafi wa mazingira ili kutimiza malengo ya kuuweka mji huo katika hali ya usafi.
Hayo yalibainishwa jana mjini Maswa wakati akifungua kikao maalum cha wadau wa usafi wa mazingira wilayani humo kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya hiyo na kuwashikirikisha viongozi mbalimbali.
Alisema mji wa Maswa ni miongoni mwa miji ambayo imekithiri kwa uchafu, hivyo ni vizuri wakaanzisha siku maalumu ya usafi wa mazingira kila juma.
“Mji wetu kwa kweli ni miongoni mwa miji ambayo imekithiri kwa uchafu, hivyo ni vizuri tukaanzisha siku maalum ya kufanya usafi wa mazingira, kila juma tutaanza katika mji wa Maswa na baadaye zoezi hili litaendelea wilaya nzima,” alisema.
Alisema takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya asilimia 70 ya magonjwa yanayotibiwa katika vituo vya afya nchini, yanahusiana na uchafuzi wa maji na mazingira.
Aliyataja madhara mengine kuwa ni pamoja na kuathiri mandhari ya makaazi ya watu kutokana na kuzagaa hovyo kwa uchafu wa kila aina ukiwemo taka ngumu kama mifuko ya plastiki, harufu mbaya inayotokana na kuoza kwa taka na maji machafu yanayotiririka hovyo.
Hata hivyo alisema ili suala la usafi wa mazingira liweze kudumu ni bora sasa sheria ya usafi wa mazingira ikaweka msisitizo kwa ulipaji wa faini ya papo kwa hapo kwa kila mkazi anayekamatwa akitupa uchafu katika maeneo yasiyoruhusiwa.
Pia alitumia nafasi hiyo kuwaonya viongozi wa kisiasa kuacha kutumia nyadhifa zao kuingilia kazi ya usafi wa mazingira kwani kufanya hivyo ni kuwarudisha wananchi nyuma kimaendeleo.
Naye ofisa mtendaji wa mamlaka ya mji mdogo wa Maswa, Rogers Lyimo, alisema kutokana na ongezeko la kasi la watu katika mji huo sambamba na ukuaji wa sekta binafsi hasa maeneo ya kibiashara, kwa sasa mji huo umekuwa ukizalisha zaidi ya tani 15 kila siku za uchafu.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa