Home » » Vijana watakiwa kuchangamia fursa zinazojitokeza

Vijana watakiwa kuchangamia fursa zinazojitokeza



VIJANA katika wilaya ya Busega, mkoani Simiyu, wametakiwa kuchangamkia fursa zinazojitokeza kwenye maeneo yao, ili waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na umasikini.

Ushauri huo umetolewa jana na mwenyekiti wa wilaya mpya ya Busega, Bw. Lukale John Charles, katika mji mdogo wa Lamadi, wilayani Busega wakati akifungua semina ya kuwapa uwezo vijana ili waweze kujua wajibu wao kama vijana, elimu ya ujasiriamali, kujua sera ya vijana, uongozi na stadi za maisha.

Bw. Charles amesema kuwa vijana ni nguzo ya taifa hivyo wanafaa kuwezeshwa, ikiwa ni pamoja na kuchangamkia fursa zinazojitokeza ili waweze kuondokana na umasikini.

Amesema kuwa vijana wanazo fursa nyingi lakini wamekuwa wakishindwa kuzitumia fursa hizo, na badala yake kusingizia serikali kwamba haijawafanyia chochote.

Aidha amewahimiza vijana kukazania elimu kwani njia pekee ya kujiondoa kwenye lindi la umasikini ni elimu, ambayo ndio msingi wa maisha.

Amesema kuwa kwa sasa serikali kupitia wizara ya habari, utamaduni, vijana na michezo, imetenga kiasi cha shilingi bilioni 6.1 ambazo zitawekwa kwenye saccos za vijana za wilaya husika na kwamba ni vema sasa vijana wakachangamkia hiyo fursa kwa kuanzisha benki hiyo na kujiunga kwenhe vikundi ili waweze kupata mkopo wa fedha hizo.

Awali mkurugenzi mtendaji kutoka wizara ya habari, utamaduni, vijana na michezo, Dk. Kisusi Stevin Kisusi, amesema kuwa vijana ni muhimu sana katika jamii na taifa kwa ujumla, hivyo ni vema wakaijua sera yao, badala ya kukalia kulalamika kwamba serikali bado haijawafanyia chochote.

Bw. Kisusi amesema kuwa vijana ambao ni milioni 16.2 wakiwemo wanawake  milioni 6.3 na wanaume milioni 7.9 sawa na asilimia 35 ya watu wote na asilimia 68 ya nguvu kazi ya taifa, inapaswa waisome na kuijua sera yao, juu ya wajibu wao na serikali kwa ujumla.


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa