Home » » UNUNUZI WA PAMBA WASUASUA

UNUNUZI WA PAMBA WASUASUA

na Samwel Mwanga, Simiyu
KUSUASUA kwa ununuzi wa Pamba wilayani Maswa Mkoa mpya wa Simiyu kumewasikitisha viongozi wa wilaya hiyo licha ya kuwepo kwa kampuni 10 zilizoidhinishwa na Bodi ya Pamba (TCB) kufanya kazi hiyo msimu huu.
Masikitiko hayo yalioneshwa jana na Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Luteni msataafu Abdallah Kihato na Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Hilda Lauwo, wakati wa kikao maalumu cha kuhakikisha pamba yote wilayani humo imenunuliwa kabla ya mvua za vuli.
Katika hali ya kushangaza wakuu hao wamedai kusikitishwa na kasi ndogo ya makampuni yaliyopewa vibali vya kununua zao hilo kuwakopa wakulima na kukwepa ushuru wa halmashauri hiyo wa asilimia mbili badala ya asilimia tano kwa mujibu wa agizo la serikali.
Agizo hilo la serikali limetokana na kudorora kwa biashara ya pamba kwenye soko la dunia.
Luteni Kihato alisema licha ya wakulima kukubali kuuza pamba yao kwa sh 660 bado kampuni hizo zimeshindwa kuinunua na kujikuta wakimkopa mkulima na kusababisha malalamiko kutoka kwa wakulima.
Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo alisema amechanganyikiwa, hasa akizingatia maelekezo anayopewa na madiwani kukusanya ushuru na kufikia malengo yaliyowekwa, huku wanunuzi hao wakikwepa kulipa hata ushuru wa asilimia mbili.
Miongoni mwa wajumbe waliokuwemo kwenye kikao hicho ni Mbunge wa Maswa Mashariki, Slyvester Kasulumbayi, Katibu wa Mbunge wa Maswa Magharibi, Ziadah Hamisi, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Steven Dwese, Mkurugenzi wa Huduma za Usimamizi wa Bodi ya Pamba Tanzania, James Shimbe na Mkurugenzi wa Bodi hiyo Kanda ya Ziwa, Jones Bwahama.
Wilaya ya Maswa inatarajia kununua kiasi cha kilo milioni 35,000 za pamba msimu huu na kujipatia zaidi ya shilingi bilioni 1.7 za ushuru wa pamba mbegu, ikilinganishwa na zaidi ya kilo 8,000,000 zilizonunuliwa msimu uliopita 2011/12.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa