Home » » CHAVITA yaiomba Serikali kuandaa mkakati wa kuwawezesha walimu wa lugha ya alama.

CHAVITA yaiomba Serikali kuandaa mkakati wa kuwawezesha walimu wa lugha ya alama.

 
Na Beatrice Lyimo-MAELEZO
 
 
Dar es Salaam.
CHAMA cha Viziwi Tanzania (CHAVITA)chaiomba Serikali kuandaa mkakati wa kuwawezesha walimu wa lugha ya alama kupata utaalamu wa kuweza kufundisha watoto viziwi kutumia lugha hiyo.

Mwenyekiti wa chama hicho Bw. Nadrosy Mlawa aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam kuhusu maadhimisho ya wiki ya viziwi duniani ambapo kitaifa yanafanyika mkoani Tanga.

Bw. Mlawa  alisema kuwa mbali na hali ya maendeleo ya viziwi kuimarika kutokana na kukua kwa  mwamko katika jamii na Serikali kwa ujumla pamoja na  ushiriki wa wadau mbalimbali katika harakati za watu wenye ulemavu ambao  wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo kutokuwa na wataalamu  wa kufundisha watoto viziwi nchini.

“Kwa sasa hali ya maendeleo kwa viziwi inazidi kuimarika kutokana na kukua kwa mwamko katika jamii na serikali kwa ujumla, ushiriki wa wadau mbalimbali katika harakati za watu wenye ulemavu umesaidia kuimarisha hali hii tofauti na miaka ya 1990” alisema Bw. Mlawa

Aidha, aliendelea kufafanua kuwa jamii imekuwa ikiunga mkono juu ya matumizi ya lugha ya alama na kupenda kujifunza lugha hiyo ya viziwi, pia kumekuwa na baadhi ya taasisi ambazo zinajali mahitaji ya viziwi na kuchukua hatua ya utekelezaji wa mahitaji hayo.

Mbali na hayo, Mwenyekiti huyo alisema kuna changamoto nyingi wazipatazo viziwi kutegemeana na hali halisi ya mazingira, umri na shughuli wazifanyazo ikiwemo kutofundishwa kwa lugha ya alama katika ngazi zote za upatikanaji wa elimu.

Vilevile ukosefu wa huduma ya ukalimani kwenye maeneo na matukio nyeti yanawafanya viziwi kufadhaika na kuonekana kuwa hawawezi, hawaelewi, wagumu na kutowajibika licha ya baadhi yao kuwa na taaluma mbalimbali.

Bw. Mlawa aliendela kwa kusema kuwa kutotambuliwa kirahisi na utamaduni wa kiziwi anayetumia lugha ya alama na kubambikiwa majina yanayodhalilisha utu ni miongoni mwa changamoto wanazokumbana nazo katika jamii.

Kwa upande wake Mratibu kutoka Chama cha Walimu wenye Uziwi Tanzania Francis Mbisso alisema kuwa pamoja na uwepo wa mikakati, sheria, kanuni na programu zenye matamko chanya bado utekelezaji wake unasuasua kwa baadhi ya maeneo nchini.

Alisema kuwa shule za viziwi na vitengo vya viziwi zimekuwa zikikosa ufundishaji wa watoto viziwi kwa kutumia lugha ya alama ikiwa na sababu kubwa ya walimu kukosa utaalamu wa lugha hiyo na kutegemea kujifunza kutoka kwa wanafunzi wao.

Mbali na hayo alitoa wito kwa jamii kwa ujumla wakiwemo waandishi wa habari kujifunza lugha ya alama ili kuweza kuwasaidia na kuwapasha habari zinazohusu jamii na huduma nyingine.

Wiki ya viziwi duniani huadhimishwa kila mwaka  mwezi Septemba ikiwa na lengo la kuonyesha jamii uwezo wa viziwi na kuelemisha jamii changamoto wazipatazo kutokana na hali ya ulemavu wao na jisni ya kuzishughulikia.
mwisho
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa