Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Rubani, Roger Gower.
Washtakiwa wanne waliofikishwa Mahakama ya Wilaya ya
Bariadi kwa mara ya kwanza Februari 10, mwaka huu kwa kosa la kutungua
helikopta 'chopa' na kusababisha kifo cha rubani wake, Roger Gower, raia
wa Uingereza katika pori la akiba la Maswa wilayani Meatu, wamehukumiwa
kifungo cha miaka 15 jela kila mmoja baada ya kupatikana na hatia ya
makosa manne.
Makosa hayo ni kukutwa na bunduki mbili aina ya Riffle 303 na 458 pamoja na risasi sita.
Waliohukumiwa kifungo hicho mbele ya Hakimu Mkazi wa wilaya, Mary
Mliyo, ni Mange Buluma (47), Shija Mjika (38), Dotto Pangali (41) na
Njile Gunga (28), ambao wamehukumiwa kutumika kifungo cha miaka 15 jela
kila mmoja kwa kosa la pili kati ya makosa 11 waliyoshtakiwa.
Awali mbele ya Hakimu Mliyo, Wakili wa Serikali, Yamiko Mlekano na
Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Koplo Edwin Alphonce, katika kesi
iliyotajwa Februari 10, mwaka huu, iliahirishwa hadi jana baada ya
kuwasilishwa vielelezo vya kesi hiyo.
Mlekano alisema washtakiwa hao wote wamekutwa na hatia na kukiri
kutenda makosa hayo kinyume cha sheria ikiwa ni pamoja na kupatikana na
risasi sita.
Alisema kwa mujibu wa ushauri wa mkuu wa upelelezi wa mkoa huo,
kuwa kukutwa na bunduki na risasi siyo kosa, lakini kubwa ni kukutwa na
silaha pasipo na kibali cha umiliki, hivyo washtakiwa hao walionekana
kutokuwa na nia njema kwa usalama wa watu na mali zao.
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Mliyo alidai kwa mujibu wa sheria
iliyopitishwa na Bunge, Novemba 2015 na kufuta iliyotangulia, adhabu ni
haki ya kisheria na lengo la adhabu ni kuonya na washtakiwa hao
hawakuisumbua mahakama sambamba na kukiri makosa yao, hivyo mahakama
inawahukumu kifungo cha miaka mitano kwa kila kosa, hivyo kutumikia
miaka 15 kila mmoja kwa makosa matatu kuanzia la pili, la tatu na la
nne.
Hata hivyo, katika kosa la tano, washtakiwa Dotto Pangali na Njile
Gunga, walihukumiwa kulipa faini ya Sh. milioni 10 kwa kila mmoja au
kutumikia kifungo cha miaka mitano kwa kosa la kukutwa na risasi moja ya
bunduki ya Riffle 303 ambayo ilitumika kuua tembo.
Hakimu Mliyo alisema kesi hiyo iliyokuwa na washtakiwa tisa,
wengine walikana makosa yao yakiwamo ya kukutwa na silaha na risasi
ambao ni, Mange Buluma, Moses Masasi na Mwigulu Kanga, hivyo kurudishwa
mahabusu na kesi yao itaendelea Februari 24, mwaka huu.
CHANZO:
NIPASHE.
0 comments:
Post a Comment