Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Na Richard Mabala
Katika karne ya kumi na tisa, kulikuwa na mwandishi mmoja wa
Urusi aitwaye Tolstoy. Aliandika riwaya bora sana, pia alikuwa
mwanafalsafa aliyependa sana usawa, ingawa yeye mwenyewe tajiri na
aliyechukia sana matumizi yoyote ya nguvu na ukatili.
Kutokana na umaarufu wake, alipata wafuasi wengi.
Sasa kichekesho ni kwamba hatimaye wafuasi walikuwa na nguvu kuliko
Tolstoy mwenyewe, hasa pale alipoanza kuzeeka.
Hivyo, walichambua kila alichoandika hata kabla
hakijachapishwa kisha kukibadilisha, eti kinaenda kinyume na Utolstoy
wake. Yeye ndiye Tolstoy, lakini wao waling’ang’ania kufinya utolstoy
wake hadi ufanane na walichotaka wao. Na waliweza kufanya hivyo kwa
sababu walikaa kwake, walikula kwake na kufaidi matokeo yote ya uandishi
bora wa Tolstoy.
Mwishowe Tolstoy wa watu akiwa na takriban miaka
tisini, alilazimika kujaribu kutoroka nyumbani kwake ili apate uhuru.
Alitoroka usiku na kufanikiwa kufika mbali kidogo, lakini afya yake
ikamsaliti, akaugua na ikabidi arudishwe nyumbani na kufariki muda mfupi
baadaye.
Hapo sasa. Hata sisi wengine tunabadilika na kuwa
na mawazo na misimamo mipya kidogokidogo kutokana na kusoma zaidi,
kujadili zaidi na kupata mikasa na uzoefu mbalimbali katika maisha yetu
na kama tuko tayari kutumia akili yetu, hasa kutafakari kuhusu hayo yote
tuliyosoma, kujadili na kupitia. Na iwapo ni hivyo kwetu, nadhani ni
zaidi kwa watu ambao umaarufu wao unatokana na kutafakari zaidi, kusoma
zaidi, kupata uzoefu zaidi na kadhalika. Utamfinyaje mtu kama huyu
badala ya kumwachia aendelee kutafakari kwa kina zaidi na kuona mengine
ambayo yanaweza kutufikirisha zaidi?
Tutamlaanije mtu, eti amebadili mawazo kama vile
kubadili mawazo ni kufisadi au kuua? Kubadili mawazo ni sehemu ya
ubinadamu wetu na ingawa wengine wanabadili kutokana na pochi tu, siyo
haki kumshambulia kila mtu aliyebadilika kwa kuwa pochi imetawala. Hata
kutobadili mawazo kunaweza kutokana na pochi pia.
Nadhani ndiyo maana Waswahili hupenda kusema
‘wapambe nuksi’. Licha ya mambo mengine ya kujipendekeza na kutaka
kumfaidi mtu, wao daima wanapamba ya jana wakati mtu ameshasonga mbele
zaidi leo. Akitaka kusonga mbele zaidi, wanamvuta nyuma ili afuate yayo
hayo. Hii ndiyo maana ya uhafidhina wa kijinga. Dunia inabadilika,
lakini wanataka sote tugande kama vile tuko katika friza. Mwisho wa
mawazo mgando ni kifo cha mawazo.
Naam, najua wengine watamcheka Tolstoy aliwezaje
kutawaliwa hivyo na kushangaa wale waliomfinya kwa kujidai ni wajuzi
kuliko yeye, lakini mbona sisi tunafanya vilevile. Angalia wapambe nuksi
wa dini ambao wako tayari kuchukua neno moja la waanzilishi wa dini zao
na kulitumia kuwaangamiza watu wengine huku neno hili likigongana
kabisa na maneno elfu yenye wazo tofauti.
Tunachukua yale tu ambayo tunayataka sisi. Ndiyo
maana wengine wanasema si kweli Mungu alituumba kwa mfano wake. Sisi
wapambe nuksi tunamwumba (na kumwumbua!) kwa mfano wetu.
Kwa nini naongelea yote hayo? Nimesoma habari
ambazo siwezi kuziamini. Siwezi kuamini kwamba, licha ya kujaribu
kufinya maneno na busara hai ya baba wetu wa taifa, watu wanataka
kumfinya na kumtia kwenye friza kama vile hakubadilika na yeye. Na sasa
wanathubutu kumfinya hata mjane wake.
Nani anaweza kusahau wakati wa kufariki kwa baba
yetu, jinsi alivyoagwa na wananchi wake hadi alipozikwa? Lakini katika
kumbukumbu zangu zote, kuna moja ambayo inanigusa hadi moyoni kila
nikiifikiria.
Baada ya watu wote kumaliza vyao, namkumbuka Mama
Maria akienda huko kaburini ambapo tayari ilikuwa imefunikwa. Akapiga
magoti mbele yake na kutandaza mkono wake juu ya kaburi. Kilikuwa ni
kitendo kidogo, lakini kitendo kilichobeba maana pana na ya kina kabisa.
Hicho kitendo kilibeba maumivu yake yote ya kumkosa mwenzake,
pamoja na mshikamano wake naye hadi kaburini. Mtu aliyeona hilo aliweza
kuhisi ukaribu wa mama na baba. Waliishi pamoja, waligawana maoni yao,
walijitolea kujenga taifa badala ya tumbo, hadi kweli wakawa wamoja kwa
namna ambayo simenti ya kaburi haiwezi kabisa kuwatenganisha.
Wanaosoma makala zangu wanajua kwamba siyo kawaida
yangu kutaja jina la mtu, lakini leo sina budi kufanya hivyo maana
ninamheshimu Mama Maria kupita kiasi.
Sote tunajua kwamba yeye siyo msemaji sana ndiyo maana akisema, tunatega sikio kwa nguvu zote, maana maneno yake ni tunu kwetu.
Sasa, alichosema juzi kuhusu mustakabali wa taifa
letu siyo la kupuuza hata kidogo. Ndipo hapo tunaingia kwenye mambo ya
wafuasi wa Tolstoy. Wapambe nuksi watakana alichosema na kujaribu
kuponda na hata kuficha alichokisema, lakini maneno yake ni hai kuliko
yao.
Halafu bado siamini, yaani haiingii akilini,
lakini sijaona anayekanusha, eti mama yetu wa taifa anaamriwa asome
magazeti hadi analazimika kumtuma mtu kupata magazeti anayotaka yeye,
lakini ambayo wapambenuksi hawataki aone. Hivi kuna ujinga zaidi ya huu?
Kuna udhalilishaji zaidi ya huu? Kuna ukiukwaji wa haki za watu kuliko
huo? Tena kwa mama wa taifa.
Lakini la kushangaza ni kwamba hata magazeti
hawajaamka na kulaani vikali kunyimwa kwake haki ya kupata taarifa. Hivi
ni wapambe nuksi na wao au wamefinywa? Mbona hakuna ufuatiliaji?
Ingekuwa Makengeza amenyimwa magazeti sawa, lakini Mama wa Taifa?
Haiyumkiniki.
Hata hivyo, imenikumbusha jinsi ofisi zetu
zinavyopambwa na magazeti ambayo sisi tulio wengi hatusomi. Sijui ni
katika mkataba kwamba lazima waweke gazeti la Serikali na la chama
tawala tu, lakini sielewi sababu yake. Msingi wa demokrasia siyo kufinya
mawazo ya watu bali kupanua, ila iwapo lengo ni kufanya watu wasinzie
wakati wanasubiri basi wamefanikiwa sana.
Hivyo, siwezi kumshauri mama yetu naye ajaribu
kutoroka kama Tolstoy, lakini nadhani ni muhimu sana tuhakikishe kwamba
yeye, pamoja na sisi sote wengine tunapata habari za uhakika, tunapata
haki yetu ya kusoma vyanzo mbalimbali ili tuweze kutumia akili yetu
kuchambua.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment