Home » » MASWA WAKATAA VIONGOZI

MASWA WAKATAA VIONGOZI


WANANCHI WA wa Wilaya ya Maswa, mkoani Simiyu, wamemkataa Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Hilda Lauwo na Mwenyekiti wa Halmashauri, Stephen Dwese kwa madai ya kukwamisha maendeleo.
Tukio hilo lilitokea juzi katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya hiyo katika kikao cha pamoja cha majumuisho ya ziara ya siku mbili ya Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri, aliyoifanya wilayani hapa na kuwashirikisha wadau mbalimbali.
Wananchi walitoa dukuduku hilo baada ya Naibu Waziri huyo kuwapa nafasi ya kuuuliza maswali na kutoa maoni yao juu ya uendeshaji wa halmashauri hiyo.
Walilalamikia uongozi mbovu wa mkurugenzi Lauwo, ambao umesababisha shughuli za maendeleo kutofanyika kwa kiwango kinachotakiwa huku wakimtupia lawama Mwenyekiti Dwese kuwa ndie chanzo cha mambo yote kutokana na kumkumbatia mkurugenzi huyo.
Kutokama na hali hiyo, wananchi hao walimtaka Naibu Waziri huyo akiondoka Maswa aondoke nao, kwani hawawafai.
“Naibu Waziri ukimaliza ziara yako hapa Maswa uondoke na mkurugenzi na mwenyekiti wa halmashauri kwani hawa ndio wanaokwamisha shughuli za maendeleo wilayani kwetu. Mkurugenzi ana kiburi na jeuri na hii yote inatokana na kukingiwa kifua na Mwenyekiti Dwese, mie nadai zaidi ya sh milioni 30, nilijenga vyumba vya madarasa katika Shule ya Msingi Igongwa sasa ni miaka 11 nazungushwa na viongozi hawa,” alisema Edward Bunyongoli huku akishangiliwa na wananchi.
Walisema licha ya halmashauri kupata hati safi, lakini kwa hali halisi Mkurugenzi Lauwo hana mahusiano mazuri na baadhi ya wakuu wa idara, jambo linalosababisha shughuli za maendeleo kutokusonga mbele.
Hata hivyo, Mwenyekiti Dwese alipotakiwa kutolea ufafanuzi jambo hilo na Naibu Waziri, alijikuta akijibiwa kwa sauti na kelele za wananchi waliohudhuria mkutano huo kuwa ni mwongo huku wakisisitiza aondoke nao.
Akijibu hoja hizo, Mwanri alieleza kushangazwa na baadhi ya viongozi kutojali kero za wananchi hali ambayo inawafanya wanachi waichukie serikali.
“Nataka niwaeleze bayana kuwa ukiona unasemwa au unalalamikiwa huo ndio wakati wa kusikiliza na sio kuwachukia wanaokulalamikia… nawapongeza wananchi wanaoeleza wazi udhaifu wa viongozi, mambo haya yasiposhughulikiwa ndiyo yanayosababisha wananchi kuichukia serikali,” alisema.
Hata hivyo, alikanusha madai kuwa na undugu na Mkurugenzi Lauwo.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa