Home » » Kamani apania wanaodhulumu wafugaji

Kamani apania wanaodhulumu wafugaji

WAZIRI wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Titus Kamani, amesema atapambana na majambazi na wanaodhulumu wavuvi na wafugaji ili kukomesha tabia hiyo.
Alisema hayo juzi alipokuwa akiwahutubia mamia ya wananchi waliofika katika viwanja vya Lamadi kwa ajili ya mapokezi baada ya hivi karibuni kuchaguliwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa waziri wa wizara hiyo.
Kamani alisema atahakikisha anazunguka maeneo mbalimbali nchini, ili kubaini watu wanaowanyonya wafugaji, wavuvi na kushughulika nao huku akiongeza kuwa hakuna sababu ya watu hao kuwa maskini wakati kuna rasilimali za kutosha.
“Nashangaa sana kwanini nchi iwe maskini, kwanini wafugaji wawe maskini au wavuvi wawe maskini wakati tuna maziwa makubwa, kama vile Natron, Victoria, Eyasi, Nyasa, Tanganyika na mito huku kukiwa na mifugo mingi, lakini wanaohusika na rasilimali hiyo wakiendelea kuwa maskini zaidi. Hili jambo haliwezani,” alisema.
Kamani ambaye pia ni mbunge wa Busega, alisema ametokea katika familia ya wavuvi na wafugaji, na kwamba hiyo kazi ataiweza kwa kuifanya kwa vitendo, hivyo Watanzania wanatakiwa kumpa moyo na nguvu ili aweze kufanya kazi inavyotakiwa.
Alieleza kuwa yeye si kiongozi wa maneno, anachohitaji ni vitendo na utekelezaji, hivyo hatomvumilia kiongozi anayeendekeza malumbano na wizi wa fedha katika idara yoyote inayomuhusu kuisimamia hata katika halmashauri anayotoka.
Mbunge wa Kahama, James Lembeli, alisema anamfahamu Dk. Kamani tangu alivyokuwa naye Tanapa, na kwamba kama rais angemchagua ‘mzigo’ asingetokea kumuunga mkono na kumpokea jimboni kwake
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa