Home » » MTU MMOJA AHUKUMIWA KUNYONGWA HADI KUFA

MTU MMOJA AHUKUMIWA KUNYONGWA HADI KUFA


na Samwel Mwanga, Simiyu


MAHAKAMA Kuu Kanda ya Tabora imemhukumu, Njile Ntemba (37), mkazi wa Kijiji cha Mwagai, Wilaya ya Meatu, Mkoa wa Simiyu, kunyongwa hadi kufa baada ya kupatikana na hatia ya kuua kwa kukusudia.
Akitoa hukumu hiyo jana katika Mahakama ya Wilaya ya Maswa, Jaji wa mahakama hiyo, Haruna Songoro, alisema kuwa upande wa mashitaka umethibitisha bila kuacha shaka kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo.
Ntemba alipatikana na hatia hiyo baada ya kushitakiwa kwa kumuua, Magreth Benjamin (55), mkazi wa kijiji hicho ambaye alikuwa mkwewe, kwa kumkatakata kwa mapanga, tukio lililotokea majira ya saa 8:00 usiku, Agosti 18, 2007.
Ilidaiwa mahakamani hapo mbele ya Jaji Songoro na Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Denis Kamara, kuwa mshitakiwa alimvamia marehemu nyumbani kwake wakati amelala na kumkatakata kwa mapanga, hatua iliyosababisha kifo.
Wakati huo huo, Mahakama Kuu Kanda ya Tabora inayoendelea na kikao chake katika mahakama ya wilaya hiyo imemhukumu, Sami Clement (32) kifungo cha miaka tisa jela baada ya kupatikana na hatia ya kuua bila kukusudia.
Ilidaiwa kuwa mshitakiwa alimuua Tiho Shagembe (70) mkazi wa Kijiji hicho kwa kumpiga na jembe kichwani na kumsababishia kifo baada ya kumtuhumu kuwa ni mshirikina.
Tukio hilo lilitokea Mei 16, 2007 katika Kijiji cha Gambosi, Wilaya ya Bariadi, Mkoa wa Simiyu.
Akitoa hukumu hiyo, Jaji Haruna Songoro alisema kuwa upande wa mashitaka umethibitisha kuwa mshitakiwa alitenda kosa hilo na adhabu hiyo iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia hiyo.

CHANZO TANZANIA DAIMA

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa