Home » » KIMBUNGA CHAVURUGA MWENGE

KIMBUNGA CHAVURUGA MWENGE



na Samwel Mwanga, Maswa
UPEPO mkali uliozuka ghafla katika uwanja wa Nguzo Nane ulioko wilayani Maswa, Simiyu wakati wa sherehe za mapokezi ya Mwenge wa Uhuru umesababisha watu kadhaa kujeruhiwa wakiwemo wanafunzi baada ya mahema yaliyokuwepo eneo hilo kuezuliwa.
Tukio hilo lilitokea juzi, majira ya saa 10:45 jioni wakati wa risala ya utii ya wananchi wa Wilaya ya Maswa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikisomwa na Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Danford Peter.
Wakati risala hiyo ikisomwa, ghafla upepo mkali maarufu kwa jina la kimbunga ulitokea na kuezua mahema yaliyokuwepo huku vyuma vikiwaangukia baadhi ya watu na kuwasababishia majeraha.
Waliojeruhiwa katika tukio hilo ni Pastory Elias (16), aliyejeruhiwa kichwani na mkono wa kulia, Justine Abdu (12) aliyejeruhiwa mkono wa kulia, Chausiku Selemani (14) aliyejeruhiwa mkono wa kushoto na mmoja aliyejulikana kwa jina moja la Juma aliyejeruhiwa mkono wa kushoto wote wakiwa ni wanafunzi wa shule za msingi walioalikwa kwenye sherehe hiyo.
Wengine ni Juma Hassan (26) aliyejeruhiwa sehemu ya shingoni na mkono wa kushoto na Edward Salvatory (45) aliyejeruhiwa sehemu ya bega lake la kulia na kuchomwa na kitu chenye ncha kali.
Kutokana na tukio hilo, hotuba hiyo ilisitishwa kusomwa kwa muda huku Kiongozi wa mbio za Mwenge, Luteni Honest Mwanosya, akiwa makini kuhakikisha Mwenge huo haupati madhara yoyote ikiwemo kuzimika.
Jumla ya miradi yenye gharama ya sh bilioni 3.6 ilizinduliwa katika sherehe hizo, ikiwamo ya elimu, afya, maji, maliasili na mazingira.
Chanzo: Tanzania Daima



0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa