Home » » Wanafunzi waacha shule kuuza pombe

Wanafunzi waacha shule kuuza pombe



na Sitta Tumma, Bariadi
WILAYA ya Bariadi mkoani Simiyu, imetajwa kuwa ni miongoni mwa wilaya zinazoongoza kwa wanafunzi wake kuacha masomo na kwenda kuuza pombe za kienyeji na hivyo kuporomoka kwa elimu wilayani humo.
Mbali na hayo, imeelezwa kwamba ajira za utotoni, baadhi ya viongozi wa vijiji kutosimamia vema shughuli za kimaendeleo katika maeneo yao, ushirikiano mbovu baina ya watendaji na wananchi na makato makubwa ya mishahara ya walimu, ni chanzo kikuu cha kukwamisha maendeleo.
Kauli hiyo ilitolewa juzi mjini Bariadi na walimu kutoka sehemu mbalimbali wanaoshiriki warsha ya siku tatu ya 'Chukua Hatua', iliyoandaliwa na Taasisi ya Kutetea na Kujenga Demokrasia na Utawala Bora (ADLG).
Wakichangia mada ya kero katika sekta ya elimu, walimu hao walisema wanafunzi wengi wamekuwa wakiacha masomo kisha kujihusisha na biashara ya uuzaji wa pombe, jambo linalodidimiza ukuaji wa maendeleo ya sekta hiyo.
Kwamba hata baadhi ya viongozi wa ngazi za vijiji na wizara husika wameonekana kushindwa kuwachukulia hatua za kisheria wazazi wa wanafunzi hao.
Walisema kuwa ili kuondoa tatizo hilo na hatimaye wilaya hiyo kupiga hatua kubwa za kimaendeleo, ni vema viongozi wa ngazi zote wakashirikiana pamoja kupambana na hali hiyo mbaya, ikiwa ni sambamba na kuwachukulia hatua kali za kisheria wazazi ama walezi wanaoshindwa kusimamia maendeleo ya elimu kwa watoto wao.
“Wanafunzi wengi wanaingia darasani wakiwa na njaa. Kwa maana hiyo uelewa unakuwa mdogo sana, maana wengi wanasinzia na kushindwa kusoma vizuri,” alisema mmoja wa walimu hao.
Aidha walimu hao walikwenda mbali zaidi na kusema kwamba hulka ya baadhi ya wazazi na walezi kuwaoza watoto wao wa kike, unywaji wa pombe baina ya walimu wakati wa kazi ni kikwazo pia cha upatikanaji wa maendeleo, na kwamba baadhi ya wananchi wa vijiji husika wamekuwa wakiendekeza ubaguzi wa kabila kwa walimu.
Awali, Mkurugenzi wa ADLG, Jimmy Luhende, alisema lengo la warsha hiyo ni kuwapatia elimu ya uwajibikaji walimu wa shule mbalimbali katika wilaya sita za mikoa ya Simiyu, Shinyanga na Geita.
CHANZO MTANZANIA DAIMA


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Simiyu Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa